Image

Katika zama hizi za utandawazi na muingiliano baina ya tamaduni zetu za asili na tamaduni za kimagharibi, imekuwa ni kawaida kwa vijana wa rika tofauti na jinsia zote kutoga ulimi, mdomo, kitovu ama kivimbe cha nyusi kwa sababu tofauti tofauti sana.

Hivyo basi, ni muhimu sana kufahama ukweli kuhusu faida ama hasara za kutoga ulimi ama mdomo kabla hujatekeleza azma yako ya kutoga viungo hivi vya mwili.

Kutoga Ulimi ama Mdomo kunaweza kukusababishia madhara yasiyotarajiwa

Matokeo mazuri zaidi ya kutoga ulimi ama mdomo ni kutokutokea kwa kidonda ama kivimbe, wakati matokeo mabaya kutokea kwa baadhi ya watu ni pamoja na kuvunjika kwa meno/jino, kuvuja kiasi kikubwa cha damu, ama maambukuzi ya bakteria kwenye kidonda. Kutoga ulimi hujumuisha kutumika kwa sindano inayopenyezwa katikati ulimi ili kupitisha na kuhifadhi kipini, ama ndoana ama hereni ya urembo. Kazi hii ya kutoga ulimi mara nyingi ganzi huwa haitumiki. Baada ya kutoga, kuvimba kwa ulimi na maumivu ya muda hutokea.

Madhara ya kutoga Ulimi

  • Kuvuja damu kiasi kidogo hutarajiwa, kuna hatari ya mishipa ya damu kuharibiwa wakati wa kutoga ulimi, hali inayoweza kusababisha kuvuja damu kwa kiasi kikubwa kuliko ilivyotarajiwa.
  • Ingawa kuvimba kwa ulimi kunatarajiwa baada ya kitendo cha kutoga ulimi, wakati mwingine ulimi huvimba kwa kiasi cha kuziba kwa njia ya hewa. Kuziba kwa njia ya hewa kunaweza kusababisha kifo.
  • Ikiwa fundi wako wa kutoga ulimi hana uzoefu wa kutosha kufanya kazi hiyo, anaweza kuharibu mishipa ya fahamu ya ulimi hivyo kuharibu uwezo wa ulimi kuhisi/kutambua hisia za joto,baridi ama ladha ya chakula na vinyaji, vile vile kuathiri mienendo ya viungo vya eneo la kinywa na uso. Kwani nyuma ya ulimi kuna mishipa ya fahamu,mishipa hii ikiharibiwa ulimi utapooza hivyo kusababisha ganzi la kudumu, kuathirika kwa uwezo kuongea na kushindwa kutambua ladha za chakula/vinywaji
  • Vilevile kutoga ulimi kunakuweka kwenye hatari ya kupata maambukizi kwenye ulimi hasa ikiwa hutaweza kutunza hali ya usafi wa kinywa na meno kila wakati, hivyo kusababisha wadudu jamii ya bakteria kupenya na kuingia ndani ya ulimi na kusababisha maambuzi kwenye ulimi.
  • Hali ya kutoga ulimi inapodumu kwa muda mrefu, inaweza kusababisha nyufa kwenye meno, ama kuvunjika kwa nyuso za jino/meno kwa sababu ya msuguano wa muda mrefu kati ya jino/meno na hereni/kipini ama ndoana ya chuma/plastiki iliyohifadhiwa kwenye ulimi kwa muda mrefu. Nyufa hizi kwenye meno, kwa kawaida husababisha maumivu makali ya jino/meno. Hivyo basi meno haya yenye nyufa yanaweza kutibiwa kwa kuvalishwa kofia “ dental crown”. Si kawaida kupata magonjwa ya fizi ama kuta za ndani za shavu ikiwa umetoga ulimi na unatunza afya ya kinywa na meno vizuri.

Kutoga Mdomo

Kutoga mdomo ni pale pete ya urembo inapovalishwa ama kuhifadhiwa ndani ya mdomo. Majeraha ya kutoga mdomo hupona haraka zaidi, hata hivyo unapaswa kutunza kidonda cha jeraha hili kwa umakini mkubwa wakati wa kupona. Vyakula, vinywaji na moshi wa sigara vinapofikia kidonda hiki, vinaongeza hatari ya kupata maambukizi kwenye kidonda.

Kishikizo vishikizo vya pete hii ya urembo kinaweza kusababisha vidonda kwenye fizi ama kuharibu jino. Kwa baadhi ya watu, tiba ya kupandikiza fizi hutumika kurejesha fizi zilizoathirika. Kama ilivyo kwa kutoga ulimi, kutoga mdomo pia kunaweza kuathiri mshipa wa fahamu hivyo kuathiri mienendo ya misuli  ya kwenye eneo la kinywa na mdomo.

Je, una mpango wa kutoga Ulimi ama Mdomo?

Ikiwa unapanga kutoga viungo hivi vya mwili, unashauriwa ufanye mambo yafuatayo yatakayo kuwezesha kupata huduma ambayo haita athiri afya yako:

  • Hakikisha ngariba mtoga ulimi ama mdomo sio tu ana uzoefu wa kutosha kwenye kazi anayofanya, bali pia anazingatia usafi kufanya kazi zake.
  • Nenda hospitali kupata ushauri tiba mara tu unapoona ama maumivu ni makali sana, kuvimba kwa ulimi ama damu zinavuja kwa muda mrefu (zaidi ya dakika 30) ama ikiwa jeraha linapata maambukizi ya bakteria.
  • Unapokuwa na hereni, pete ama ndoana ya urembo kwenye ulimi ama mdomoni, unashauriwa kumwona daktari wa kinywa na meno kila baada ya miezi sita (6). Daktari wa meno atafanya kazi ya kuhakiki ikiwa kidude kilichovalishwa kina madhara kwenye meno ama fizi, hivyo kudhibiti athari zinazoweza kutokea kwa kutoga ulimi ama mdomo.
  • Wana michezo wanashauriwa kutovaa hereni, pete ama ndoana ya urembo iliyopo kwenye ulimi ama mdomoni wanapokuwa mchezoni, kwani vyombo hivi vya urembo vinaweza kunasa kwenye ngozi bila kutarajia hivyo kusababisha madhara yasiyotarajiwa.
Imesomwa mara 29134 Imehaririwa Jumatatu, 26 Novemba 2018 09:16
Dr. Barnabas Mbogo

Dr. Barnabas Mbogo ana utaalamu kwenye meno na programu za afya ya jamii kwa ujumla(Community Health Programs))

Anwani ya barua pepe hii inalindwa kutokana na spambots. JavaScript lazima iwe itawezeshwa kwa kuweza kuona.